Monday, July 17, 2017

TPDC yawaita wawekezaji wa viwanda

ad300
Advertisement

 
Mhandisi Kapulya Musomba

NA WILLIAM SHECHAMBO

SHIRIKA la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC), kama yalivyo mashirika mengine ya umma hapa nchini, limekiri kuwa na mchango mkubwa kwenye kuifikia Tanzania ya viwanda inayolengwa na serikali ya awamu ya tano.

Mchango huo ni kulingana na nafasi yake inayopewa uzito na shughuli zake zilizoko kwa mujibu wa sheria Sheria ya Mashirika ya Umma Namba 17 ya mwaka 1969 ya sheria za Tanzania ilioondolewa na kubadilishwa na Kifungu Namba 257 cha Sheria ya Mashirika ya Umma cha mwaka 2002 cha Sheria za Tanzania.

Kifungu hiko kwa kupitia notisi ya Serikali Namba 140 ya Mei 30 mwaka 1969, Shirika hili lilianza shughuli rasmi mwaka 1973 chini ya usimamizi wa msajili wa hazina na baadaye lilikabidhiwa kwa Wizara ya Nishati na Madini.

Shughuli kuu za shirika kwa wakati huo zilikuwa ni kusimamia shughuli za kampuni ya Mafuta ya AGIP - Azienda Generale Italiana Petroli ambayo ni Kampuni ya Mafuta ya Italia.

Shughuli za utafutaji mafuta na gesi asilia nchini zilianza miaka ya 1950 kupitia Kampuni hiyo ya Agip kutoka Italia ambapo licha ya shughuli hizo kuanza miaka ya 1950, ilifanya ugunduzi wa kwanza katika Kisiwa cha Songo Songo mkoani Lindi mwaka 1974 ambao ulifuatiwa na ugunduzi mwingine katika eneo la Mnazi Bay (Mtwara) mwaka 1982.

Hata hivyo, historia inaonesha kwamba gesi hiyo asilia haikuendelezwa kwa kuwa ilionekana haina  manufaa ya kiuchumi kwa nchi wakati huo kutokana na teknolojia kuwa bado chini.

Baada ya ugunduzi huo, TPDC iliendelea kufanya utafiti ikiwa ni pamoja na kuchimba visima mbalimbali kwa ajili ya kuthibitisha kiasi cha gesi asilia kilichopo katika maeneo ambako gesi asilia iliyogunduliwa.
Ilipofika Novemba mwaka 2014, kiasi cha gesi asilia kilichogunduliwa nchini kilielezwa kuwa ni futi za ujazo trilioni 53.28 (53.28TCF), ambazo kwa mujibu wa wataalamu akiwemo aliyekuwa Waziri wa Nishati na Madini kwa wakati huo, Profesa Sospeter Muhongo, kilikuwa ni kiasi kikubwa cha kumaliza matatizo ya nishati nchini.

Serikali katika kuhakikisha kuwa inanufaika na rasilimali ya gesi asilia
iliyogunduliwa, kupitia TPDC ilianza utekelezaji wa mradi wa ujenzi wa mitambo mbalimbali ya kisasa.

Mitambo hiyo ilijumuisha ile ya kusafisha gesi asilia katika maeneo ya Madimba mkoani Mtwara na kule Songo Songo, Lindi sambamba na bomba la kusafirisha gesi asilia hiyo kutoka Mtwara, kupitia Somanga Fungu (Lindi), Pwani mpaka Dar es Salaam.

Kwa mujibu wa serikali lengo la kutekeleza miradi hiyo ni kuhakikisha
kuwa gesi asilia mbali na matumizi mengine,  itumike katika kuzalisha umeme ambao kwa sasa unazalishwa kwa kutumia mafuta ambayo ni ghali.

Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa TPDC, Mhandisi Kapulya Musomba, anathibitisha kufanikiwa kwa lengo hili la serikali kwamba kwa sasa, kiasi cha fedha zinazotumiwa na serikali kuagiza mafuta ya mitambo ni asilimia chini ya 1 kutoka gharama za awali zilizokuwa Dola za Marekani Bilioni 1 kila mwaka.

“Hii ni kutokana na kwamba sasa hivi gesi iliyopo nchini inatosheleza matumizi ya mitambo iliyohitaji mafuta awali na kwa bahati nzuri mitambo mingi mikubwa inayoingizwa nchini siku hizi ikiwemo ile ya TANESCO ina sehemu ya kutumia gesi,” anasema.

Mkurugezi huyo anasema umma unapaswa kufahamu kwamba TPDC ni kitovu cha Tanzania ya viwanda kwa kuwa viwanda vinahitaji nishati ya umeme ili vifanye kazi na katika hilo, hadi sasa asilimia 50 ya umeme wa Shirika la Umeme Tanzania inazalishwa kutokana na gesi asilia.

Anasema tangu kuingia madarakani kwa serikali ya awamu ya tano, TPDC imeendelea na kasi ya kutekeleza mikakati yake ikiwa ni pamoja na kushiriki na kujiingiza katika utafiti, maendeleo, uzalishaji na ugawaji wa mafuta na gesi na huduma zinazohusiana na hayo.

Pia kuweka mazingira mazuri ya biashara, kulinda mgawanyo wa taifa wa mazao ya mafuta ghafi na wakati huo huo kuendeleza ubora na kiwango cha usalama kwa kulinda watu, mali na mazingira.

Si hayo tu, anaeleza kuwa lengo ni kudhihirisha mtazamo wao kama shirika ambao ni kuongoza kwenye ushindani wa kitaifa, kimataifa katika hali ya kujali mazingira kwa faida ya wadau wote huku ikiendelea na kutekeleza wajibu wa shirika kwa taifa, ambao miongozo yake ipo kisheria.

Kuhusu suala la mchango wa TPDC na maendeleo ya viwanda hapa nchini, anasema mfano hai ni pale shirika lilipotangaza kutoa nafasi ya kupokea maombi kwa viwanda kuunganishiwa nishati ya gesi asilimia.

Anasema kwa kipindi kifupi walipokea maombi ya viwanda takriban 47 kutoka mkoa wa Dar es Salaam na Pwani huku Pwani ikiongoza kwa kuwa na maombi mengi ya viwanda takriban 44.

Pia anasema wana mpango wa kusambaza gesi asilia kwenye mikoa mingine hususan Dodoma na Tanga ambako ili kufika huko ni lazima mikoa mingine ipate jambo linalofanyiwa utafiti kwa sasa ili ujenzi wa miundombinu uanze.

Pamoja na hayo anafafanua kuwa kutoka Mtwara mpaka Dar es Salaam kuna eneo la kilomita za eneo zaidi ya 540 ambazo ziko wazi kwa uwekezaji wa viwanda vikubwa na ambalo linafikiwa kwa ukaribu na bomba kubwa la gesi asilia hivyo fursa za uwekezaji zipo na nishati ya uhakika.

“Unaweza kuona kuwa kutokana na kazi inayofanyika siku hizi watanzania wanaanza kusahau matatizo ya umeme kwa sababu nishati inazaliwa kwa wingi.

“Kwa mfano awali tulizoea umeme unakatika hata saa saba mpaka 10 kwa siku na watu wanaona sawa tu lakini leo nusu saa umeme ukikatika ni malalamiko kila kona ya nchi,” anasema.

Mkurugenzi huyo wa TPDC anasema mbali na viwandani, shirika liko kwenye mpango wa kusambaza gesi asilia kwenye makazi ya watu kama ilivyoeleza awali, ambapo inafungua milango kwa wawekezaji washirikiane na TPDC kuwekeza kwenye mradi huo.

“Lengo ni kutunza mazingira kama inavyofahamika kwamba mkaa unachangia kwa kiasi kikubwa uharibifu wa mazingira na kwa kiasi kikubwa wananchi wengi wanatumia nishati hii,” anafafanua.

Hata hivyo anasema changamoto kubwa ni kwamba utaratibu wa kufunga miundombinu ya gesi 
asilia si kwa mitungi bali ni mifumo ya mabomba ambayo kutokana na namna ilivyo kwa ujenzi wa kitanzania kazi kubwa ya kitaalamu inatakiwa kufanyika ili kufanikisha hilo.

Katika kueleza mipango ya kuuza gesi nje ya nchi kwa hali ya kimiminika na kuongeza kipato cha taifa anasema kiwanda kitajengwa mkoani Lindi muda wowote huku mradi wa bomba la mafuta kutoka Uganda kuja Tanzania ukiwa kwenye hatua ya makadirio ya awali ikiwemo kuwalipa wananchi.

“Tunaamini ifikapo mwaka 2020, mafuta ya kwanza kutoka nchini Uganda yataanza kuingia Tanzania kwa sababu tayari wakuu wetu wa nchi hizi mbili wameshasaini mikataba ya kuruhusu mradi huu mkubwa kuanza rasmi,” anasema.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Bodi ya TPDC, Profesa Sufian Bukurura, anasema nishati ya gesi ina unafuu wa bei kulinganisha na nishati yoyote ya jamii za mafuta hivyo mchango wa TPDC kwa maendeleo ya viwanda nchini ni mkubwa.

Anasema TPDC kwenye kuonesha mchango wake wa moja kwa moja kwenye uchumi wa viwanda unaowekewa msisitizo na serikali iliyopo madarakani unadhihirika kwa faida wanayoipata wawekezaji wa viwanda mkoa wa Pwani.

“Mkoa wa Pwani hasa wilaya ya Mkuranga amabyo ndio ina viwanda vingi vikubwa vilivyokamilika, una bahati kwamba bomba la gesi limepita hivyo moja ya kiwanda cha mfano ni Goodwill Ceramic, ambacho ni cha kwanza kuunganishiwa gesi kutoka bomba letu kubwa,” anasema.

Aidha anasema TPDC ina ushirikiano mzuri wa wakazi wa vijiji vyote vinavyopitiwa na bomba kuu la gesi lakini ni wajibu wa kila mwananchi kwa nafasi yake kutambua kuwa wajibu wa kutunza miradi ya serikali iliyoigharimu nchi fedha nyingi inatunzwa na kila mtu.

“Unaweza usilipwe fedha lakini kwa kutoa taarifa unapoona mtu mwingine anahujumu miradi ya gesi, unakuwa umeokoa kuangamiza taifa lako na kizazi chako kijacho kwa miaka mingi ijayo,” anafafanua Profesa huyo.

Wananchi wao wanasema ni dhahiri kuwa TPDC lina mchango mkubwa wa kuitoa kimasomaso Tanzania kwenye uchumi wa viwanda, kwa sababu bila nishati ya uhakika hakuna viwanda wala treni za mwendo kasi.

“Wafanye kazi, waepuke mikataba pori kama ile ya Acacia, wawe macho ili gesi na mafuta vipatikane vikauzwe kwa bei halali nje ya nchi na hapa nchini zitumike ipasavyo kulishia viwanda maendeleo tuyaone hata kabla ya 2020,” anasema Felician Kolimba.

Juma Kilowoko anasema viwanda vyote vikubwa nchini havipaswi kutumia umeme wa maji na badala yake vifungiwe mifumo ya umeme wa gesi asilia ili ule wa maji uende kwa wananchi pekee.

Anasema kama ilivyofanywa kwenye mvutano baina ya serikali na kiwanda cha Aliko Dangote, Machi mwaka huu, TPDC chini ya Wizara ya Nishati, viwanda vingine vikubaliane juu ya bei ya mauziano ya gesi asilia kwa ajili ya matumizi ya viwanda na kukuza uchumi wa taifa kwa kuuza bidhaa nje ya nchi.
Share This
Previous Post
Next Post

Pellentesque vitae lectus in mauris sollicitudin ornare sit amet eget ligula. Donec pharetra, arcu eu consectetur semper, est nulla sodales risus, vel efficitur orci justo quis tellus. Phasellus sit amet est pharetra

0 comments: