Thursday, February 1, 2018

TMA, UK Met Office wawanoa wanahabari wa mwambao wa bahari ya Hindi

ad300
Advertisement
Dk. Hamza Kabelwa akizungumza kwenye ufunguzi wa warsha 
Mamlaka ya Hali ya Hewa Nchini (TMA), kwa kushirikiana na Shirika la Hali ya Hewa la Uingereza (UK Met Office) wanafanya warsha ya wanahabari jijini Tanga, kwa madhumuni ya kufanyia kazi mapendekezo ya watumiaji wa bahari katika suala zima la kutoa taarifa za utabiri za tahadhari za awali za mabadiliko ya hali ya hewa.

Akifungua warsha hiyo ya siku mbili kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu wa TMA, Dk. Agnes Kijazi, Mkurugenzi wa Huduma za Utabiri wa TMA, Dk. Hamza Kabelwa amesema warsha hiyo ina lengo la kuongeza nafasi ya TMA kutoa taarifa za haraka na uhakika kwa watumiaji wa bahari kwa kupitia vyombo vya habari.

Dk. Kabelwa amesema kwa kipindi kirefu TMA wamekuwa wakishirikiana na vyombo vya habari kote nchini, vikiwemo vile vya kijamii ili kusaidia jamii ya kitanzania iweze kupata taarifa za mabadiliko ya hali ya hewa ambazo kiuhalisia ni mtambuka na zina manufaa makubwa kwa maendeleo ya jamii na taifa kwa ujumla.

Amesema kwa kushirikiana na ofisi ya hali ya hewa ya Uingereza, wamefanya utafiti mdogo ambao umedhihirisha kuwa uhitaji wa taarifa za hali ya hewa ni mkubwa  kwa watumiaji wote wa bahari ambapo wengi walihitaji ufahamu wa kasi na nguvu ya upepo, hali ya anga na nyakati za kupwa na kujaa kwa maji.

Mkurugenzi huyo pia alitumia fursa hiyo kuwashukuru UK Met kwa ushirikiano wao wa hali na mali katika kufanikisha utendaji wenye ufanisi wa Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania huku pia akiwataka wanahabari waliohudhuria warsha hiyo kushiriki kikamilifu ili kutekeleza kwa vitendo kile ambacho TMA na UkMet wanakilenga kwa jamii kupitia kazi za vyombo vya habari.

Kwa upande wake mwakilishi wa UK Met, Becky Venton amesema ofisi yao imekuwa ikifanya kazi kwa karibu na TMA lengo likiwa ni kusaidia utoaji wa tahadhari na taarifa za hali ya hewa kwa jamii na kwamba wataendelea kufanya hivyo kwa manufaa ya jamii kwa ujumla.

Warsha hiyo pia inakusanya maoni na mapendekezo ya wanahabari juu ya mfumo mpya ambao TMA inakusudia kuanza kuutumia ambao unahusisha utoaji taarifa za utabiri wa hali ya bahari wa siku tano kwa mara moja.

Warsha hiyo imehudhuriwa na wanahabari kutoka mikoa takriban mitano iliyoko pembezoni mwa bahari ya Hindi na visiwa vya pemba na Unguja na watumishi kutoka TMA na Ofisi ya Waziri Mkuu kitengo cha maafa.


Mwakilishi wa UK Met Becky Venton akitoa maelezo ya awali kabla ya kuanza kwa warsha hiyo.

Baadhi ya washiriki ambao ni waandishi wa habari wakiwa kwenye majadiliano.

Hellen Msemo wa Mamlaka ya Hali ya Hewa akiwasilisha mada kwenye warsha hiyo ya wanahabari.


Warsha ikiendelea katima hoteli ya Mkonge, Jijini Tanga.

Baadhi ya watumishi wa Ofisi ya Waziri Mkuu, kitengo cha Maafa.


Share This
Previous Post
Next Post

Pellentesque vitae lectus in mauris sollicitudin ornare sit amet eget ligula. Donec pharetra, arcu eu consectetur semper, est nulla sodales risus, vel efficitur orci justo quis tellus. Phasellus sit amet est pharetra

0 comments: