Thursday, February 1, 2018

Wizara yafafanua upatikanaji wa Cheti cha taaluma baada ya kupotea/kuharibika kwa kile cha awali

ad300
Advertisement
NAIBU Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, William Ole Nasha, amefafanua utaratibu wa kupata cheti mbadala/uthibitisho kwa mtu aliyepoteza cheti ambapo ameeleza kuwa Baraza la Mitihani litafanya kazi hiyo kwa muda usiozidi siku 30.

Ole Nasha aliyasema hayo bungeni mjini Dodoma alipokuwa akijibu swali la Mbunge wa Mafinga Mjini, Cosato Chumi (CCM) lililokuwa likihoji utaratibu unaotumika pale mtu anapopoteza cheti ili aweze kupata cheti kingine.

"Je, unapata cheti halisi au nakala na ni taratibu gani anatakiwa kuzifuata mhusika ili ombi lake lifanyiwe kazi ipasavyo na bila kucheleweshwa?," aliuliza.

Katika majibu yake Naibu Waziri huyo alieleza kuwa mhitimu aliyepoteza cheti hupatiwa cheti mbadala/uthibitisho wa matokeo kwa kutoa taarifa kwa Jeshi la Polisi kuhusu upotevu wa cheti na kupata hati ya upotevu.

Alisema mtu aliyepotelewa na cheti atatakiwa kutangaza gazetini kuhusu upotevu huo  kwa lengo la kuutaarifu umma ili kusaidia kukipata na endapo cheti hakitapatikana hata baada ya kufuata utaratibu huo, mhitimu atatakiwa kujaza fomu ya ombi la cheti mbadala /uthibitisho wa matokeo na kuiwasilisha Baraza la Mitihani (NECTA).

‘’Baada ya mhitimu kujaza fomu hiyo Baraza la Mitihani hufanya uchunguzi wa uhalali wa umiliki wa cheti husika na kutoa huduma stahiki ,wahitimu waliofanya mtihani kuanzia Mwaka 2008 ambao vyeti vyao vina picha hupatiwa vyeti mbadala,‘’ alisema.

Pia aliongeza “Na waliofanya mtihani kabla ya Mwaka 2008 hupatiwa uthibitisho wa matokeo ambao hutumwa kwa waajiri wao au mahali pengine kwa mahitaji yaliyotolewa na mwombaji na kundi hilo halipewi cheti mbadala.’’

Alisema cheti mbadala kinachotolewa ni cheti halisi ambacho huongezwa maandishi yanayosomeka ’DUBLICATE’ kuonyesha kuwa cheti hicho kimetolewa mara ya pili.
Share This
Previous Post
Next Post

Pellentesque vitae lectus in mauris sollicitudin ornare sit amet eget ligula. Donec pharetra, arcu eu consectetur semper, est nulla sodales risus, vel efficitur orci justo quis tellus. Phasellus sit amet est pharetra

0 comments: