Monday, February 5, 2018

Dk. Kigwangallah- Sipokei ombi kufuta eneo la hifadhi

ad300
Advertisement
WAZIRI wa Maliasili na Utalii Dk. Hamis Kigwangallah amesema hatajibu maombi yoyote yaliyowasilishwa ofisini kwake kutoka kwa walio chini yake, ambayo yanayohusu kufuta  maeneo ya Hifadhi ili yatumike kwa ajili ya  matumizi mengine.

Amesema maeneo hayo yalitengwa kisheria na yana umuhimu mkubwa kiuchumi na kijamii hivyo lazima yaendelee kuhifadhiwa kwa ajili ya faida ya  kizazi cha sasa na kijacho hivyo mwenye mamlaka ya kumfanya abadili uamuzi huo ni aliyemteua pekee.

"Katika kipindi  cha Uwaziri wangu, sitajibu ombi lolote lile linalohusu kubadili matumizi ya maeneo hayo kwa vile kuwa na misitu sehemu za mijini ni sehemu ya maendeleo," alisema.

Aliyasema hayo mjini Iringa alipokuwa akizungumza  kwa mara ya kwanza na kamati ya kitaifa ya ushauri wa misitu iliyokutana kwa ajili ya kufanya kikao chake cha tatu tangu ilipoundwa mwaka jana.

Hatua hiyo iliambatana na kutembelea msitu wa Hifadhi wa Kihesa Kilolo uliiombwa na uongozi wa mkoa kufutwa ili upate kutumika kwa kuweka miundo mbinu mipya ya mji wa kitalii.

Katika kikao hicho ambacho Mkuu wa mkoa wa Iringa, Amina Masenza alishiriki, Waziri Kigwangallah  aliyeambatana na Naibu waziri wake, Japhert Hasunga alimuomba Mkuu  huyo awafikishe ujumbe   Wakuu wa mikoa wengine  ambao walituma na wanaotarajia kutuma maombi ya namna hiyo kuwa yeye  hatayajibu hadi pale  aliyemteua atakapompa maelekezo na si  vinginevyo.

Alisema halmashauri nyingi nchini kila zikiona maeneo ya Hifadhi zimekuwa zikifikiria kubadili matumizi ya  maeneo hayo ili yatumike kwa shughuli zingine za maendeleo kama vile  kupima viwanja  ili  kuwauzia wananchi kwa lengo la kukusanya mapato.

"Ofisini kwangu kuna  maombi mengi mno ambayo hata sielewi nianze na lipi na niache lipi, nasema sitajibu ombi lolote lile" alisisitiza Waziri Kigwangallah.

Aidha,  Waziri Kigwangallah   mara baada ya kuzungumza na kamati hiyo alitembelea eneo la hifadhi ya msitu huo  huku  akiwa ameongoza na kamati hiyo  pamoja na Uongozi wa Mkoa wa huo.

Wakati akitembelea eneo hilo, Waziri Kigwagwallah aliwashangazwa na kitengo cha viongozi wa halmashauri  kuanzisha dampo   katika  eneo hilo  huku kamati ikijionea magari matatu ya taka  yakiendelea kumwaga uchafu kwenye eneo hilo jambo ambalo ni  kinyume na sheria za uhifadhi.

Naye Naibu Waziri wa Wizara hiyo, Japhet Hasunga  aliwashukia watendaji wa mkoa huo  wakati  walipokuwa  wakipishana kutoa maelezo kuhusiana na mipaka na matumizi ya eneo hilo endapo Wizara  itaridhia ombi lao la  kubadili matumizi ya eneo hilo.

Kufuatia hali hiyo,  Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Amina Masenza  alimuhakikishia Waziri kuwa eneo hilo endapo watapewa litatumika kwa malengo yaliyokusudiwa na si vinginevyo.

Waziri Kigwangallah mara baada ya kutembelea eneo hilo wakati akitoa majumuisho yake, alisema kufuatia ziara hiyo anasubiri ushauri utakaotolewa na kamati ya kitaifa ya msitu ndipo atakapokuwa na  jibu kuhusiana na ombi  la kubadilia matumizi la eneo hilo .

Pia, Waziri Kigwangallah  aliiagiza ofisi ya Mkuu wa Mkoa kuhakikisha kuwa  maeneo ya  milima kwa vile sio moja ya  maeneo ya hifadhi  yaongezwe katika eneo la hilo  lengo   likiwa ni kuzuia uharibifu wa uoto wa asili unaoendelea katika maeneo hayo.

Awali,  Mwenyekiti wa Kamati hiyo wakati akitoa neno la shukrani alimhakikishia Waziri kuwa watamshauri jambo lolote lile  linalohusu misitu bila kujali litamfurahisha au litamuudhi, kitakachoangaliwa hapo  ni maslahi mapana ya taifa.

Katika hatua nyingine ,Waziri Kigwangallah  ameitaka Wakala wa Huduma za Misitu nchini  (TFS)  kuanza kuweka nguvu nyingi katika kuhifadhi misitu baadala ya kuvuna na kufanya biashara ya mazao ya misitu.

Alisema licha ya kuwa TFS imekuwa ikifanya vizuri katika baadhi ya maeneo  lakini katika suala la kuhifadhi misitu imekuwa kama vile  sio kazi yake: "TFS yenyewe kazi yake imekuwa  ni  kuvuna kilichopandwa, kuuza na kukusanya mapato yatokanayo na mazao ya misitu" alisema. 

Wakati huo huo, Waziri Kigwangallah amesema Wizara inakusudia kuchukua misitu yote iliyo chini ya vijiji na Halmashauri kwa vile zimeshindwa kuisimamia ipasavyo na hivyo kupelekea sehemu kubwa ya nchi kugeuka kuwa jangwa.

Mbali na hilo amewaonya wananchi wanaowazuia watendaji  kuweka alama za vigingi katika mipaka ya hifadhi, huku wengine wamekuwa wakiving'oa na wengine kuhamisha vigingi hivyo kutoka eneo moja hadi jingine kuwa  waache tabia hiyo kabla hawajachukuliwa hatua kali za kisheria.
Share This
Previous Post
Next Post

Pellentesque vitae lectus in mauris sollicitudin ornare sit amet eget ligula. Donec pharetra, arcu eu consectetur semper, est nulla sodales risus, vel efficitur orci justo quis tellus. Phasellus sit amet est pharetra

0 comments: