Tuesday, August 29, 2017

TASAF yasaidia 121 kujiunga na Bima ya Afya Mbinga

ad300
Advertisement
Wanufaika 121 wa Mpango wa Kunusuru Kaya Masikini unaoratibiwa na TASAF katika kijiji cha Kilindi, kilichopo kata ya Matiri wilayani Mbinga, mkoa wa Ruvuma wamejiunga na mfuko wa bima ya afya.

Akizungumza na Blog hii ofisini kwake leo Agosti 29, Ofisa Mtendaji wa kijiji hicho, Maula Komba, alisema wanufaika hao baada ya kuhamasishwa juu ya umuhimu wa kujiunga na mfuko huo kwa pamoja waliridhia kutekeleza hilo.

Walisema sehemu ya fedha zao waliamua kulipia bima hiyo hali ambayo imekuwa msaada mkubwa kwao pindi wanapougua na kulazimika kwenda katika zahanati, kituo cha afya au hospitali.

Maula alisema kabla ya uamuzi huo wa kujiunga na bima ya afya wanufaika wa mpango huo wa kunusuru kaya masikini walikuwa wakikosa uwezo wa kulipia huduma za matibabu jambo ambalo wakati mwingine lilikuwa likipelekea baadhi yao hata kupoteza maisha.

Baadhi ya wanufaika hao wakiwemo Osiana Kapinga na Imelda Milinga, waliipongeza serikali kwa kutekeleza vizuri mpango huo wa kunusuru kaya masikini hivyo kusababisha jamii hiyo iondokane na matatizo makubwa waliyokuwa wakikumbana nayo kwa muda mrefu ikiwemo kuwa na uhakika wa kupata huduma bora za matibabu pindi wanapougua.

Joyce Ngatunga na Augeni Hyera nao walisema kitendo cha wao kuhamasishwa kujiunga na bima ya afya kutawafanya waweze kuendelea na kazi za uzalishaji mali kwa umakini mkubwa kutokana na ukweli kwamba sasa wanauhakika wa kupata matibabu bure kwa kipindi kirefu.

"Sasa fedha tunazozipata badala ya kuzielekeza kwenye huduma za matibabu zitakuwa na kazi moja tu ya kusaidia katika mapambano dhidi ya umasikini wa kipato kupitia kilimo na shughuli zingine za kiuchumi," alisema Joyce.

Walisema wamekuwa wakinufaika na mpango huo tangu awamu ya kwanza ambapo fedha walizozipata waliamua kuanza kufuga kuku ambao kwa sasa wamefikia 60 kutoka kuku kumi waliowanunua awali.

Kwa upande wake mratibu wa TASAF wilayani Mbinga, Ahsante Luambano, alisema jumla ya Sh. bilioni 4.8 zimetolewa katika kipindi cha kuanzia Julai 2015 hadi Julai 2017 ambapo kaya 10,122 kutoka vijiji 108 zimenufaika na fedha hizo kwa kuanzisha miradi mbalimbali ya maendeleo.
Share This
Previous Post
Next Post

Pellentesque vitae lectus in mauris sollicitudin ornare sit amet eget ligula. Donec pharetra, arcu eu consectetur semper, est nulla sodales risus, vel efficitur orci justo quis tellus. Phasellus sit amet est pharetra

0 comments: