Tuesday, August 29, 2017

Nishati na Madini yatoa mafunzo ukusanyaji maduhuli ya serikali - GePG

ad300
Advertisement


Wizara ya Nishati na Madini imetoa mafunzo ya Mfumo wa pamoja wa Kukusanya Maduhuli ya Serikali (GePG) kwa Maafisa Madini na Wahasibu wa Wizara hiyo ili kuboresha shughuli za ukusanyaji maduhuli.
 
Akizungumza wakati wa ufunguzi wa mafunzo hayo, Mhasibu Mkuu wa Wizara ya Nishati na Madini, Anthony Tarimo alisema kuwa mafunzo yamelenga kuwawezesha washiriki kuuelewa vyema mfumo huo ili kuwa na ukusanyaji wa maduhuli ya Serikali wenye tija.
 
Tarimo alisema serikali imeamua kuboresha mfumo wa ukusanyaji wa maduhuli kuwa wa kielektroniki ili kurahisisha ukusanyaji wa maduhuli na vilevile kuongeza uwazi miongoni mwa Wizara na Taasisi mbalimbali za Serikali.

“Kupitia mfumo huu, Serikali inao uwezo wa kujua maduhuli yote yanayoingia kwa wakati mmoja kwa sababu umeunganishwa na Wizara na Taasisi mbalimbali,” alisema Tarimo.

Aidha alibainisha kuwa Mfumo huo wa GePG ulianza kutumika rasmi Julai, 2017 na kwamba kwa upande wa Wizara ya Nishati na Madini mafunzo ya awali yalitolewa kwa watumishi wa Ofisi ya Madini- Kanda ya Mashariki ambayo inahusisha ofisi za madini za Dar es Salaam, Pwani, Tanga, Handeni na Morogoro.
 
Alisema Mfumo huo ni rafiki na kwamba utaboresha na kurahisisha ukusanyaji wa maduhuli na kwamba mara baada ya mafunzo, washiriki watakuwa na uwezo wa kuutumia ipasavyo.
 
Tarimo alisema mafunzo hayo yanawahusu Wahasibu, Maafisa Leseni pamoja na watumishi wengine ambao kwa njia moja ama nyingine wanahusika na utoaji wa hati za madai za malipo mbalimbali.
 
Aliongeza kuwa, mafunzo hayo yanahusisha uwasilishaji wa mada mbalimbali kutoka kwa wataalam wa TEHAMA wa Wizara ya Fedha na Mipango na wa Wizara ya Nishati na Madini na pia yatahusisha majadiliano ili kuboresha utendaji kazi wa watumishi wanaohusika na ukusanyaji wa maduhuli.
 
“Wanasheria pia watawasilisha mada ili kuelewa vyema mabadiliko katika Sheria ya Madini ya mwaka 2010 yaliyofanyika hivi karibuni,” alisema Tarimo.
 
Mafunzo hayo ya siku nne yanafanyikia katika Chuo Kikuu cha Kilimo cha Sokoine Morogoro (SUA) kuanzia leo Agosti 28, 2017 kwa kushirikisha zaidi ya washiriki 100.
Share This
Previous Post
Next Post

Pellentesque vitae lectus in mauris sollicitudin ornare sit amet eget ligula. Donec pharetra, arcu eu consectetur semper, est nulla sodales risus, vel efficitur orci justo quis tellus. Phasellus sit amet est pharetra

0 comments: