Wednesday, August 23, 2017

Sekta ya Uvuvi na mchango wake kiuchumi

ad300
Advertisement

Moja kati ya shughuli zinazofanywa na wakazi wa maeneo ya pwani na kanda ya ziwa kwa madhumuni ya kuongeza pato la familia zao na pato la taifa kwa ujumla ni uvuvi.

Kutokana na umuhimu wake, uvuvi umepewa sifa ya kuwa sekta rasmi ambayo mchango wake kwenye ukuaji wa uchumi unatambuliwa na bajeti kuu ya serikali ya kila mwaka.

Licha ya hilo, unapozungumzia Tanzania ya Viwamda, huwezi kuacha kuitaja sekta ya uvuvi kama moja ya mzalishaji mkubwa wa malighafi za viwanda hususan vile vya nyama na usindikaji kwa ujumla.

Sekta hii kwa mujibu wa wataalamu akiwemo Reuben Shempemba, ambaye ni mhitimu wa shahada ya kwanza ya sayansi ya majini na uvuvi kutoka Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, inatoa kiasi kikubwa cha ajira, kipato, kujipatia riziki, fedha za kigeni na mapato kwa Taifa.

Anasema hana uhakika na takwimu za hivi karibuni kwenye suala zima la ajira zinazotokana na uvuvi, lakini ni moja ya sekta chache ikiwemo Kilimo na Madini ambazo zinatoa fursa nyingi za ajira rasmi na zisizo rasmi kwenye ukanda wote wa Pwani ya Tanzania na Kanda ya Ziwa.

Shaka ya Reuben kwenye takwimu za sasa inaondolewa na taarifa ya tovuti rasmi ya wizara ya kilimo, mifugo na uvuvi inayosema sekta ya uvuvi inaajiri zaidi ya watu 4,000,000 wanaojishughulisha na uvuvi na shughuli zinazohusiana na uvuvi, wakati zaidi ya waendesha uvuvi 400,000 wameajiriwa moja kwa moja kwenye sekta hii. 

Kwa upande wao, Ofisi ya Taifa ya Takwimu, inasema Mwaka  2016,  sekta  ya  uvuvi  ilikua  kwa  asilimia 4.2 ikilinganishwa  na asilimia 2.5 ya mwaka 2015.

Aidha, ulaji wa mazao ya uvuvi kwa mtu kwa mwaka ni kilo 8.0 ikilinganishwa na kilo 16.7 zinazopendekezwa na Shirika la Chakula na Kilimo la Umoja wa Mataifa (FAO, 2011).

Inasema Mwaka 2016, jumla ya tani 362,595 za samaki zilivunwa ikilinganishwa na tani  362,645 zilizovunwa mwaka 2015 ambapo kati  ya  kiasi  kilichovunwa,  tani  308,629  zilitoka maji  baridi  na  tani  53,823 kutoka maji  chumvi  ikilinganishwa  na    tani  309,922 zilizovunwa  kutoka maji baridi  na  tani  52,723 kutoka  maji  chumvi  mwaka 2015. 

"Mwaka 2016, mazao  ya uvuvi tani 39,691.46 na idadi ya samaki hai wa mapambo 65,841 iliuzwa  nje  ya  nchi  na  kuiingizia Serikali  mapato  ya  sh. bilioni 14.3 ikilinganishwa  na  mazao  ya  uvuvi  tani 40,540.95 na  idadi  ya samaki  hai  wa mapambo  42,100  iliyouzwa  nje  ya  nchi  na  kuiingizia  Serikali kiasi cha sh. bilioni 12.9 mwaka 2015," inasema taarifa hiyo ya NBS kwa mwaka 2016.

Aidha, licha ya mafanikio hayo na mchango wa sekta ya uvuvi kwenye maendeleo inaelewa kuwa kuna changamoto kubwa kutoka kwa wananchi wenyewe wanaotumia nguvu na akili zao zote kuharibu rasilimali hizo kutoka baharini kwa manufaa yao na ubinafsi.

Ili kupunguza uharamia huo kwenye mazao ya uvuvi, serikali ilipanga kufanya doria ambayo kwa mwaka  2016,  jumla  ya  doria  zenye  siku  kazi  4,328  zilifanyika  katika maeneo  mbalimbali  nchini  ikilinganishwa  na  doria zenye  siku  kazi  5,985 zilizofanyika mwaka  2015. 

Taarifa rasmi ya NBS inasema katika  doria  hizo,  zana  haramu  zikiwemo  nyavu kokoro  968,  kamba  za  kokoro  zenye  urefu  wa  mita  742,356,  nyavu  za  makila 3,096 zenye  macho  madogo; nyavu  za  dagaa  483 na nyavu  za  utali  15,753 zilikamatwa.

Nyingine ni vyandarua 33 vya mbu, nyavu za kimia 32, katuli 16, mikuki 3,408,  mabomu 17, V6  explosive  vipande  600,  Detonator  vipande  35,  tambi  za  baruti  2,  mbolea  ya urea  kilo  252, mitungi  ya  gesi  ya kuzamia  55,  mitumbwi  338,  injini  za mitumbwi  mitano. 

Watuhumiwa mbali na kukamatwa na zana hizo haramu kwa uvuvi inaelezwa walikutwa na samaki  wachanga aina ya Sangara  kilo  14,015,  sato  kilo  39,  kaa kilo  50,  kambakoche  kilo  172,  nyama  kilo  16,  majongoo  bahari  kilo  48, magamba  ya  starfish  kilo  12,  dodoji  (seahorse)  vipande  775,  makome  ya baharini  kilo  401  mapezi, mataya  ya  papa  kilo  14.5  na  matumbawe  kilo  75.

Jumla ya watuhumiwa  waliokamatwa ni 293 ambapo  kesi  21  ziliwasilishwa  mahakamani  na sh. milioni 37.7 zilikusanywa kama faini na kuiongezea serikali mapato na kujizatiti zaidi kwenye kukomesha matukio hayo kwa kutoa elimu ya usimamizi na matumizi endelevu  ya  rasilimali  za  uvuvi  kwa  wavuvi  10,000 kupitia  maonesho  ya nanenane  (Dodoma),  siku  ya chakula  Duniani  (Arusha)  na  siku  ya  uvuvi duniani  (Kigoma). 

Mbali na mafunzo hayo, wavuvi  na  wadau  wa  uvuvi  631  kutoka  Halmashauri za  Mkuranga  (93), Temeke  (130), Bagamoyo (288), Kinondoni  (130)  na  maofisa  wa  uvuvi  wilaya  kutoka  wilaya  16  za  ukanda  wa  Pwani  walipatiwa mafunzo  ya  usimamizi  wa  rasilimali  za  uvuvi  kwa  kuzingatia  mfumo  wa ikolojia na mazingira.

Changamoto hiyo ya uvuvi haramu licha ya kuonekana kuwa kubwa zaidi mtaalamu kutoka Mamlaka ya Elimu na Ufundi Stadi (VETA), anasema magugu maji ndio tatizo kubwa zaidi kwa usalama wa samaki hasa ziwani.

Mtaalamu huyo, Mashindano Lawrance, anasema kwa kutambua ukubwa wa tatizo hilo, waliamua kutengeneza mashine ya kisasa ya kuvuna magugu kutoka majini na kuyasaga kwa ajili ya kuzalisha mbolea za kilimo.

Anasema mashine hiyo imeundwa kwa umbo mithili ya boti, ambapo kazi yake kubwa ni kuangamiza mimea yote ya majini jamii ya magugu ambayo huharibu mazalia ya samaki na kupunguza idadi ya samaki majini kwa kukatisha maisha yao kabla hawajakomaa na kuzaliana.

"Magugu yanazuia uzalishaji wa samaki, kwa sababu hujifunga funga kwenye maeneo ya mazalio na kusababisha  ikolojia kuvurugika," anasema.

Anasema magugu ni hatari zaidi kwa kuwa yanasambaa kutoka sehemu moja kwenda nyingine kwa maana kwamba yana uwezo wa kuziba eneo kubwa la maji na kufanya hewa ya oksijeni isiwafikie samaki na hivyo kusababisha vifo vya samaki.

Mwisho, ni wazi hakuna asiyefahamu kwamba Tanzania imejaaliwa kuwa na maliasili nyingi za majini kwa kuwa na  jumla ya eneo la maji la bara takriban kilomita za mraba 61,500 au kiasi cha 6.5% ya jumla ya eneo la ardhi. 

Eneo hilo la maji ni kilomita za mraba 62,000 linalogawanyika kwa mgawanyiko kuwa kilomita za mraba 35,088 ni ziwa Viktoria, kilomita za mraba 13,489 ni ziwa Tanganyika, kilomita za mraba 5,760 ni ziwa Nyasa, kilomita za mraba 3,000 ni ziwa Rukwa, kilomita za mraba 1,000 ni Ziwa Eyasi na kilomita za mraba1,000 ni maeneo mengine ya maji. 

Maeneo mengi haya ya maji tafiti zinasema yana samaki wengi bila kuizungumzia bahari ambayo kwa upande wake, nchi ina bahari ya kilomita za mraba 64,000 na ukanda wa pwani wenye urefu wa kilomita 1,424. 

Ukanda Maalumu wa Kiuchumi (EEZ) unafika maili za baharini 200 katika eneo la kilomita za mraba 223,000 na kuipa nchi eneo la bahari la nyongeza na maliasili za uvuvi, hivyo wananchi hawana budi kushirikiana na serikali na mamlaka zingine kutunza utajiri huu kwa kila hali kwa maslahi ya taifa.
Share This
Previous Post
Next Post

Pellentesque vitae lectus in mauris sollicitudin ornare sit amet eget ligula. Donec pharetra, arcu eu consectetur semper, est nulla sodales risus, vel efficitur orci justo quis tellus. Phasellus sit amet est pharetra

0 comments: