Sunday, August 20, 2017

Sao Hill kuanza kuzalisha utomvu wa kutengenezea Bazooka

ad300
Advertisement
Shamba la miti la Sao Hill kwa kushirikiana na Kampuni ya Art International limeanza utafiti wa kugema utomvu wa miti ya msindano kama njia ya kujiongezea kipato.

Akizungumza na Kamati ya Bunge ya Maliasili na Mabadiliko ya tabia nchi ya nchini Malawi, iliyotembelea Shamba hilo hivi karibuni, Meneja wa Sao Hill, Salehe Beleko, alisema ushirikiano huo ni kwa lengo la kuongeza pato la shamba hilo.

"Katika kuongeza vyanzo vya mapato tumeingia mkataba na kampuni hii kufanya utafiti na ikibainika kwamba haitaathiri ukuaji wala ubora wa miti tutakuwa tumepata chanzo kipya cha mapato," alisema.

Alifafanua zaidi kuwa wanatarajia kuuza kila kilo moja ya utomvu kwa sh. 750 hivyo endapo kutakuwa na uzalishaji mkubwa shambani humo, utakuwa utajiri mkubwa kwa miaka ijayo kutokana na uhitaji wake sokoni.

Meneja huyo alisema kwa kuanzia utafiti wamelenga miti iliyokuwa tayari kuvunwa na kama wakiona hakuna madhara wataendelea kwenye miti michache yenye umri mdogo.

Alisema matokeo ya utafiti huo yatasababisha kuwepo kwa ama ruhusa rasmi ya kukuza miti hiyo kwa ajili ya kuvuna malighafi hizo ama kukataza kabisa zoezi hilo.

Naye mtaalamu wa kampuni ya Art kutoka China, Yhoung Zhoung,  alisema taasisi yake imefuata taratibu zote za ugemaji na usafirishaji wa utomvu huo.

Alisema kwamba kampuni yake inahitaji miti millioni mbili kwa mwaka ili kupata ujazo wa utomvu wanaouhitaji na kwamba watafurahi kama Sao Hill litakuwa moja ya eneo la kupata malighafi hizo.

Akijibu swali la mke wa Rais wa zamani wa Malawi, Patricia Muluzi ambaye pia ni mjumbe wa kamati hiyo, aliyetaka kujua matumizi ya utomvu huo, Yhoung alisema baada ya kuchakatwa na kuchanganywa na kemikali mbalimbali hutumika kutengenezea dawa mbalimbali, bazoka (chewing gum) na gel.

Mjumbe mwingine wa Kamati hiyo kutoka Malawi, Rashid Msusa, alisema kwa mara ya kwanza wameshuhudia matumizi mapya ya zao la mti, teknolojia ambayo hawajawahi kuiona nchini kwao Malawi.

Kamati hiyo mara baada ya kumaliza ziara hiyo Sao Hill, waliahidi kufuatilia matokeo ya utafiti huo ili kama utakuwa chanya, ikiwezekana wauhamishie Malawi ambako kuna miti ya jamii mbalimbali.

Share This
Previous Post
Next Post

Pellentesque vitae lectus in mauris sollicitudin ornare sit amet eget ligula. Donec pharetra, arcu eu consectetur semper, est nulla sodales risus, vel efficitur orci justo quis tellus. Phasellus sit amet est pharetra

0 comments: