Thursday, June 1, 2017

Bodi ya Ushauri Chuo cha Urekebishaji yazinduliwa

ad300
Advertisement
Kamishna Jenerali wa Magereza, Dk. Juma Malewa
Kamishna Jerenali wa Magereza, Dk. Juma Malewa, amezindua Bodi ya Ushauri ya Chuo cha Taaluma ya Urekebishaji Ukonga.

Bodi hiyo iliteuliwa kwa mujibu wa sheria baada ya chuo hicho kusajiliwa na Baraza la Elimu ya Ufundi Tanzania (NACTE), Juni 2015.

Itaongozwa na Mwenyekiti Dk. James Jesse, Mhadhiri wa Sheria katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), Katibu Gideon Nkana ambaye ni Mkuu wa Chuo hicho na wajumbe wengine sita.

Akizungumza kwenye hotuba ya uzinduzi jijini Dar es Salaam jana, Dk. Malewa amesema ana imani na bodi hiyo iliyoundwa na wataalamu wa sayansi ya jamii kutoka kada mbalimbali wakiwemo askari waandamizi za Jeshi la Polisi na Magereza.

Kamishna huyo amesema moja ya majukumu ya bodi hiyo ni kuhakikisha inashiriki kutatua changamoto zinazokikabili chuo hicho kichanga kinachotoa taaluma ya sayansi ya urekebishaji wahalifu na wafungwa.

Amesema kutokana na maendeleo ya sayansi na teknolojia, chuo hicho kina mikakati ya kuwa chuo cha kitaaluma katika masuala ya urekebishaji, yanayokwenda sambamba na sheria, viwango vya kimataifa ili kuandaa maofisa magereza wenye weledi.

"Hatuna shaka na uteuzi wenu, mnazo sifa, weledi na uzoefu wa kutosha ambao ni chachu ya maendeleo na mafanikio ya chuo chetu. Matarajio yetu ni kuapata mawazo yenu, mapendekezo kamwe msiache kutukosoa pale inapohitajika," amesema.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa bodi hiyo, Dk. James, amesema amepokea uteuzi wake kwa mikono miwili na kuahidi kufmshirikiana na wajumbe kufanya kazi wanayotakiwa kuifanya kwa maendeleo ya chuo hicho.

Aidha amesema amefanya kazi na jeshi la magereza kwa muda mredu hivyo anafahamu changamoto zake na kwamba atatumia muda wake na taaluma kuleta maendeleo chanya kwenye taasisi hiyo nyeti.

Mkuu wa Chuo, Gideon Nkana, amesema chuo hicho ni cha kwanza kupata usajili wa NACTE kati ya vyuo vyote vya mafunzo vilivyo chini ya jeshi la magereza na kwamba ni hatua kubwa ya kupewa kongelo.

Amesema historia ya chuo hicho inarudi nyuma mpaka mwaka 1959, kilipoanzishwa na utawala wa Mwingereza bila kuwa na dhima wala dira iliyo bayana.

"Mwaka 1968, Wizara ya mambo ya ndani iliamua kuendesha mafunzo ya idara tatu za polisi, magereza na uhamiaji kule CCP Moshi na baadaye Ukonga ikateuliwa kuandaa maofisa Magereza," amesema.

Ameongeza kuwa Juni 2015, jeshi la magereza liliamua kukisajili NACTE kwa namba REG/BTP/051, ili kiwe na uwezo wa kutoa astashahada ya msingi ya sayansi ya urekebishaji na nyingine mbili.

Kuhusu miundombinu ya chuo, amesema kina madarasa ya kutosha, maktaba, mabweni ya wanafunzi, sehemu za afya na wakufunzi wakutosha, waliobobea kitaaluma.

Chuo hicho mpaka sasa kimedahili wanafunzi 24 kwa mwaka wa masomo 2016/2017, wanaochukua kozi ya stashahada ya ufundi ya sayansi ya urekebishaji na astashahada ya ufundi ya urekebishaji.
Share This
Previous Post
Next Post

Pellentesque vitae lectus in mauris sollicitudin ornare sit amet eget ligula. Donec pharetra, arcu eu consectetur semper, est nulla sodales risus, vel efficitur orci justo quis tellus. Phasellus sit amet est pharetra

0 comments: