Monday, September 12, 2016

Dk. Shein alia na utoroshwaji Karafuu

ad300
Advertisement
Rais Ali Mohamed Shein
Zao la Karafuu ikiwa mbichi
RAIS Dk. Ali Mohamed Shein wa Zanzibar, ameviagiza vyombo vya ulinzi na usalama kushirikiana kuhakikisha waliotaka kusafirisha karafuu nje ya nchi katika bandari ndogo ya Tondooni, Mkumbuu wilaya ya Micheweni, Mkoa wa Kaskazini Pemba wanakamatwa mara moja.

Akizungumza wakati alipotembelea kituo kikuu cha karafuu cha Shirika la Taifa la Biashara Zanzibar (ZSTC) Wete jana, ili kukagua karafuu zilizokamatwa, Dk. Shein alisema uchunguzi ukifanywa kwa umakini watu hao watapatikana kwa kuwa wananchi wanawafahamu.

“Tukio hili limetushitua sote, hivyo ni wajibu wetu sote kushirikiana kuwatafuta... hawa watu wana mtandao wao na naamini wananchi wanawafahamu” Dk. Shein alisema na kusisitiza kuwa hakuna simile katika kushughulikia suala hilo.

Taarifa ya Ofisa Mdhamini wa ZSTC Pemba, Abdullah Ussi, ilieleza kuwa tarehe Septemba 3, mwaka huu, saa kumi na moja alfajiri, askari wa Kikosi Maalum cha Kuzuia Magendo (KMKM), walikamata viroba 17 vya karafuu kavu na vinne vya makonyo.

Taarifa hiyo ilibainisha kuwa baada ya uchunguzi, ilibanika kuwa karafuu hizo zilikuwa zimechanganywa na unga wa makonyo yaliyosagwa na vipande, ambapo baada ya kupimwa karafuu zilikuwa na uzito wa kilo 549 wakati unga na uchafu mwingine huo ulikuwa na uzito wa kilo 200.

Baada ya kuona uchafu huo uliochanganywana karafuu hizo, Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi alisema vitendo hivyo ni lazima vipigwe vita kwa nguvu zote kwa kuwa vinaharibu sifa za karafuu za Zanzibar.

“Huu ni uhalifu dhidi ya karafuu zetu na unahatarisha sifa ya karafuu zetu ambayo inatambulika ulimwenguni kote” Dk. Alisisitiza.

Dk. Shein alivitaka vyombo vya sheria kuwachukulia hatua zipasazo watu wanaothibitika kuhujumu zao hilo kwa kutumia Sheria ya Karafuu Namba 11 ya mwaka 2011 ambayo imebainisha adhabu mbali mbali dhidi ya watu hao.

Naye Waziri wa Biashara, Viwanda na Masoko, Balozi Amina Salum Ali, alionyesha kutoridhishwa na kasi ya hatua zinazochukuliwa dhidi ya watu wanaoshukiwa kutenda uhalifu dhidi ya zao la karafuu.

“Ni lazima uchunguzi uharakishwe ili wanaopatikana na makosa wachukuliwe hatua za kisheria ili ujumbe ufi ke kwa wahalifu wengine,” Balozi Amin alieleza.

Wakati huo huo, Shirika la ZSTC limeeleza kuwa msimu huu linatarajia kununua kiasi cha tani 2,650 za karafuu kisiwani Pemba, ambapo kati ya hizo, tani 1,500 kutoka wilaya ya Mkoani, tani 800 wilaya ya Chake Chake, tani 300 wilaya ya Wete na tani 50 wilaya ya Micheweni.

Taarifa ya Ofi sa Mdhamini wa ZSTC, Abdullah A. Ussi ilieleza kuwa hadi sasa wilaya ya Wete imeuza tani 134, sawa na asilimia 44.8 ambapo shirika hilo limekuwa na wasiwasi na kasi hiyo ndogo ya ununuzi.

Alibainisha kuwa karafuu zilizokamatwa kilo 549 ambazo baada ya kuchambuliwa zilionekana kuwa ni za daraja la tatu, zimeuzwa kwa shirika lake kwa jumla ya shilingi 5,490,000, ambazo zinashikiliwa na Jeshi la Polisi kama ushahidi katika kesi hiyo.

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi yuko kisiwani Pemba kwa ziara ya siku tatu, ambapo keshokutwa atakuwa mgeni rasmi leo katika Baraza la Eid litakalofanyika katika skuli mpya ya Mkanyageni, iliyoko wilaya ya Mkoani, Mkoa wa Kusini Pemba.

Katika hatua nyingine, Dk. Shein aliwahimiza wakulima wa karafuu kuendelea kuuza karafuu zao kwa ZSTC kwa kuwa kufanya hivyo kuna manufaa makubwa kwao binafsi na nchi kwa jumla.

Share This
Previous Post
Next Post

Pellentesque vitae lectus in mauris sollicitudin ornare sit amet eget ligula. Donec pharetra, arcu eu consectetur semper, est nulla sodales risus, vel efficitur orci justo quis tellus. Phasellus sit amet est pharetra

0 comments: