Tuesday, February 6, 2018

Naibu Gavana wa BoT alonga na Wanahabari

ad300
Advertisement
Vyombo vya habari nchini vimetajwa kuwa kiungo muhimu kwa maendeleo ya taifa kiuchumi hasa pale vinapoendelea kutumia nafasi zao vizuri kwenye kuhabarisha umma kuhusu kazi kubwa inayofanywa na serikali kwenye sekta ya fedha, biashara na uchumi.

Naibu Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania (BoT)- Utawala na Udhibiti wa Ndani, Julian Banzi alibainisha hayo alipozungumza kwenye uzinduzi wa warsha ya wanahabari wa biashara, fedha na uchumi mkoani Mtwara. 

"Mna nafasi muhimu kwenye kuisaidia nchi yetu hivyo ni vizuri badala ya kutumia muda mwingi kutumika vibaya ili kuwa chanzo cha kupiga vita jitihada nzuri zinazofanywa na serikali kwenye kuliletea taifa maendeleo endelevu mkaamua kushirikiana na wataalamu wa BoT kujua ukweli na kuuandika," alisema.

Gavana huyo alisema ni wazi kuwa vyombo vya habari vimeendelea kufanya kazi nzuri kwenye kuhabarisha umma wa watanzania juu ya maendeleo ya kiuchumi hasa wakati huu ambao taifa linauendea uchumi wa kati ifikapo 2025.

Alisema kasi ya kutekeleza wajibu huo haipaswi kupunguzwa bali iongezwe huku pia weledi, ufanisi kwenye uhabarishaji huo vikipewa kipaumbele na wanahabari wote ili kuwe na manufaa chanya badala ya upotoshaji.

"Ninawaomba wanahabari tusitumike kuhujumu jitihada za serikali, tutumie vizuri kalamu zetu lakini pale ambapo pana uozo wenye athari mbaya kwa maendeleo ya taifa letu kiuchumi hamna budi kuuibua," alisisitiza Banzi.

Alifafanua kuwa yapo mambo mengi ambayo serikali inayafanya kwa sasa na yana manufaa makubwa kwa maendeleo ya Tanzania pale itakapokamilika, hivyo ni muhimu vyombo vya habari vikayaeleza kwa umma ili kila mtu ajue serikali inafanya nini kwa ajili yake na vizazi vyake.

Banzi aliyataja mambo hayo kuwa ni pamoja na utekelezaji wa miradi mikubwa ukiwemo wa reli ya kisasa (SGR), Stingler Gorge na ujenzi wa bomba la mafuta kutoka Hoima nchini Uganda mpaka Tanga.

"Yote haya yanawasubiri ninyi muwaambie wananchi umuhimu wake kwao, fanyeni hivyo kwa sababu kuna muda mnaandika na kutangaza mambo yanayovunja moyo kweli," alisema.

Naibu Gavana huyo pia alitumia fursa hiyo ya kufungua semina ya wanahabari kuwaambia kuwa BoT inafuatilia kwa karibu taarifa zote zinazohusu masuala ya kiuchumi, biashara na masoko na kwamba wanafurahishwa na namna ambavyo wanahabari wengi wanajitahidi kuripoti kwa usahihi.

Awali, Mkuu wa Idara ya Uhusiano, Mawasiliano na Itifaki wa BoT Zalia Mbeo, alisema warsha ya mwaka huu ya wanahabari wa uchumi na fedha ni ya tano mfululizo na tayari wamepata mafanikio makubwa kwenye kujenga mahusiano mazuri baina ya vyombo vya habari na taasisi hiyo kubwa ya kifedha nchini.

Mafaniko mengine aliyoyataja kupatikana kutokana na utaratibu wao wa kutoa mafunzo ya kila mwaka kwa wanahabari alisema ni kupunguza upotoshaji wa kitakwimu na maelezo mengine kwenye habari za kiuchumi ambazo awali zilikuwa zikionekana kwa kiasi kikubwa.
Share This
Previous Post
Next Post

Pellentesque vitae lectus in mauris sollicitudin ornare sit amet eget ligula. Donec pharetra, arcu eu consectetur semper, est nulla sodales risus, vel efficitur orci justo quis tellus. Phasellus sit amet est pharetra

0 comments: