Sunday, September 3, 2017

Serikali yaagiza wavamizi Kazimzumbwi waondoke

ad300
Advertisement
Hatimaye Serikali imefunga rasmi mjadala kuhusu umiliki wa ardhi eneo la hifadhi ya msitu wa Kazimzumbwi kwa kuwaamuru wananchi waliovamia eneo hilo kuondoka haraka.

Uamuzi huo umetolewa na Wizara ya Maliasili na Utalii kufuatia kesi ya msingi iliyokuwa imefunguliwa Mahakamani na wavamizi hao dhidi ya Wizara hiyo, kuamua wananchi kuhama eneo hilo la hifadhi.

Hatua hiyo inakuja huku kukiwa na wimbi kubwa la uuzaji wa viwanja unaofanywa na wavamizi ndani ya msitu huo kwa wananchi.

Akizungumza jijini Dar es Salaam mwishoni mwa wiki iliyopita, Meneja Mawasiliano wa Wakala wa Huduma za Misitu (TFS), Glory Mziray, aliwataka wananchi  kutonunua viwanja hivyo  sambamba na kutofanya  shughuli  za kibinadamu ndani ya msitu huo.

Glory alisema wananchi watakaonunua viwanja ndani ya msitu huo watahesabika kuwa wavamizi na hatua kali zitachukuliwa dhidi yao kwa vile msitu huo umehifadhiwa kisheria.

Serikali haitamvumilia mtu yeyote atakayenunua kiwanja na kuanzisha makazi ndani msitu huo endapo utanunua ujiandae  kuondolewa  mara moja," alisisitiza.

Pamoja na hayo alisema kutokana na uharibifu unaoendelea kufanywa katika msitu huo, tayari serikali imeanza kuchukua hatua za makusudi za kuunusuru msitu huo ili usiweze kutoweka kabisa.

Moja ya jitihada hizo alisema ni utaratibu wa kuweka  vipimo vya kisasa katika msitu huo ili kuweza  kuunusuru na uvamizi pamoja na uharibifu unaofanywa na wananchi.

Alisema msitu huo umekuwa kwenye mgogoro  tangu
mwaka 1998  kutokana na kuwa karibu na makazi ya watu jambo linalochangia wakazi hao kuingia katika msitu kufanya shughuli za kibinadamu.

Migogoro hiyo iliyohusisha wananchi na walinzi wa msitu huo, ulikuwa ukichukua sura mpya kila mara, huku wananchi wakidai wana haki ya kuwepo eneo hilo na kuomba viongozi wa juu wa serikali kuwasaidia kwenye utetezi.

Msitu wa Kazimzumbwi una ukubwa wa hekta 4,860, ambapo ulitangazwa rasmi kwenye Gazeti la Serikali (GN 306) mwaka 1954.

Uwepo wake kwenye sehemu ya wilaya ya Kisarawe mkoani Pwani na wilaya ya Ilala mkoani Dar es Salaam, msitu huo umetumika kuvuta hewa chafu kutoka katika jiji la Dar es Salaam.
 
Imeandikwa na Lusungu Hellela wa Wizara ya Maliasili na Utalii na kuhaririwa na Shechambo Blog.
Share This
Previous Post
Next Post

Pellentesque vitae lectus in mauris sollicitudin ornare sit amet eget ligula. Donec pharetra, arcu eu consectetur semper, est nulla sodales risus, vel efficitur orci justo quis tellus. Phasellus sit amet est pharetra

0 comments: