Saturday, August 12, 2017

Waziri awakaba koo wapangaji JNIA

ad300
Advertisement
Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Profesa Makame Mbarawa, amewasha moto kwa wafanyabiashara waliopangisha kwenye majengo ya Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Julius Nyerere, kwa kuwapa siku 40 za kulipa madeni yao yote ya pango.

Ametoa agizo hilo alipofanya ziara kiwanjani hapo na kuzungumza na wafanyabiashara ambapo alisema pamoja na malipo hayo, serikali itapitia upya mikataba na kufanya marekebisho inapohitajika. 

Waziri Mbarawa alisema serikali ina malengo mengi kwenye kuongeza ufanisi wa viwanja vya ndege na sekta ya usafiri wa anga kwa ujumla lakini ni aibu kwamba kila fedha lazima itoke serikali kuu. 

"Tunasema hivi kwa sababu kwa viwanja vitatu yaani hapa Julius Nyerere, KIA na kile cha Mwanza kwa mwaka vinakusanya takriban Sh. Bilioni 60 au 70 hivi, wakati tuna uwezo wa kifika Bilioni 150 kwa mwaka, " alisema. 

Alisema viwanja vingi kikiwemo cha JNIA vina madeni makubwa kutoka kwa wapangaji wake ambao ni wafanyabiashara wakiwemo mawakala wa mashirika ya ndege na mawakala wa kampuni za ndani na nje ya nchi. 

"Wafanyabiashara hawa kwa maslahi ya watu wachache wasio na uzalendo, tunafahamu kuwa wanafatwa na kuombwa fedha kidogo ili deni kuu lisogezwe mbele ndio sababu mpaka leo kuna baadhi wanadaiwa kodi mpaka ya miaka mitatu au minne iliyopita. 

"Sasa nasema leo tutahitaji fedha yetu, mpaka Septemba 30 mwaka huu, hujalipa deni la pango tunakuondoa anapewa mwingine tena kwa utaratibu mzuri tu wa kutangaza na kushindanisha, " alisisitiza Waziri Mbarawa. 

Vilevile alisema lengo la maagizo hayo si kuwafukuza bali ni kufanya serikali ifaidike na uwekezaji wake na wafanyabiashara wafurahie huduma bora jambo litakalofanya viwanja vya ndege nchini viwe kibiashara badala ya kuwa kama ofisi ya kawaida ya serikali kama inavyo sasa.

Alitumia fursa hiyo pia kusikiliza kero mbalimbali za wafanyabiashara hao ambao walisema wako tayari kulipa kodi zote na tozo kama inavyoagiza serikali endapo huduma zitaboreshwa zaidi. 

Huduma walizozizungumzia ni pamoja na usalama, usafi hasa wa vyoo, uwepo wa madaktari wa dharura kwa muda wote, uharaka wa upatikanaji wa visa kwa abiria wanaowasili kiwanjani hapo na kutafuta suluhisho la muda mfupi la mlundikano wa ndege kwenye maegesho. 

Walisema kwa nyakati tofauti kwamba sehemu ya maegesho ya ndege imekuwa ndogo sana na kwamba inaleta usumbufu kwa marubani wanapotaka kuegesha ndege zao baada ya kutua. 

Aidha walisema maofisa uhamiaji kiwanjani hapi ni wachache hivyo kusababisha abiria kukwazika wanapowasili na kupoteza saa zima kusubiri huduma ya visa tofauti na ilivyo kwenye viwanja vingine vya kimataifa. 

Wafanyabiashara hao pia walitumia fursa hiyo kumuomba Waziri Mbarawa wafikiriwe kwa kupewa kipaumbele kwenye nafasi za biashara mara jengo la Terminal III litakapokamilika ujenzi wake. 

Masuala hayo yote Waziri Mbarawa aliyatolea ufafanuzi ambao uliwaridhisha wafanyabiashara hao waliopongeza jitihada zake kwa kuwajali na kuandika historia ya kufika na kuzungumza nao tangu waanze biashara kiwanja hapo.

Akihitimisha ziara yake, Waziri Mbarawa aliwaagiza viongozi wa Mamlaka ya Viwanja vya Ndege (TAA) chini ya usimamizi wa Kaimu Mkurugenzi Mkuu, Salim Msangi na Mamlaka ya Huduma za Uongozaji wa Ndege (TCAA) inayoongozwa na Hamza Johari kukutana mara kwa mara na wateja wao ili kutatua changamoto mbalimbali. 

Share This
Previous Post
Next Post

Pellentesque vitae lectus in mauris sollicitudin ornare sit amet eget ligula. Donec pharetra, arcu eu consectetur semper, est nulla sodales risus, vel efficitur orci justo quis tellus. Phasellus sit amet est pharetra

0 comments: