Friday, August 25, 2017

Profesa Mbarawa abariki Utabiri msimu wa Vuli 2017

ad300
Advertisement


Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Mhe. Prof. Makame Mbarawa (MB), ameshiriki Mkutano wa 47 wa maandalizi ya mwelekeo wa mifumo ya hali ya hewa msimu wa mvua za vuli (Oktoba-Desemba 2017) kwa Ukanda wa Afrika Mashariki na Pembe ya Afrika (Greater Horn of Africa Climate Outlook Forum-GHACOF-47).

Mkutano huo ulifanyika Zanzibar Beach Resort, Agosti 21-22, ambapo katika hotuba yake ya ufunguzi aliwapongeza wajumbe na washiriki mbalimbali wa mkutano huo kwa kuitumia sayansi waliyonayo kwa manufaa ya umma.

 “Napenda kuwapongeza GHACOF kwa kuwezesha sayansi ya hali ya hewa kutumika katika shughuli za maendeleo ya jamii, nikiangalia kwa upande wa nchi yetu ya Tanzania kumekuwa na ongezeko la mahitaji na matumizi ya huduma za hali ya hewa kwa kiasi kikubwa sambamba na wigo mpana wa uelewa wa matumizi ya taarifa hizo ambazo zitasaidia sana wananchi kukabiliana na mabadiliko ya hali ya hewa,” alisema.

Katika mahojiano yaliyofanyika na Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania, Dk. Agnes Kijazi, alielezea dhumuni la kukutana kwa wataalamu wa mkutano huo kuwa ni kujadili, kukubaliana kwa pamoja na kutoa mwelekeo wa hali ya hewa kwa msimu wa mvua za vuli kuanzia Oktoba hadi Desemba 2017 kwa Kanda ya Afrika Mashariki na Pembe ya Afrika. 

Aidha aliongezea kuwa baada ya taarifa hiyo kutolewa kila nchi shiriki ikiwemo Tanzania itakaa na kuandaa taarifa yake ambapo  kwa Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) taarifa rasmi itatolewa kwa vyombo vya habari tarehe 31 Agosti  2017.
 
Wakati huohuo, Mkurugenzi wa Kituo cha Ufuatiliaji wa Hali ya Hewa cha Afrika Mashariki na Pembe ya Afrika (ICPAC) Dk. Guleid Artan akizungumza katika ufunguzi huo alisema, ICPAC kwa kushirikiana na Shirika la Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNDP) wanatekeleza programu ya utoaji wa tahadhari na kwa wakati (Integrated Regional Early Warning System (IREWS)).

Alisema Program hiyo ina lengo la kuhakikisha nchi za Afrika Mashariki na Pembe ya Afrika wananufaika kwa kuhakikisha taarifa za hali ya hewa zitolewazo zinafika kwa jamii kwa wakati na zinatumika katika kupunguza madhara ya yatokanayo na hali mbaya ya hewa.

Naye Mkuu wa Wilaya ya Magharibi A, Zanzibar Mhe. Mwinyi Ussi Abdallah Hassan akitoa neno la shukrani kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa wa Mjini Magharibi aliwataka wananchi kufuatilia taarifa za hali ya hewa kwa karibu kwa kutumia njia za kisasa zilizopo.

GHACOF ni Mkutano unaowakutanisha wataalamu wa hali ya hewa kama watoa huduma pamoja na wataalamu kutoka katika sekta mbalimbali kama watumiaji kutoka nchi za Afrika Mashariki na Pembe ya Afrika kwa lengo la kujadili, kuandaa na kutoa mwelekeo wa hali ya hewa kwa msimu husika katika ukanda huu.

IMETOLEWA NA: MONICA MUTONI, AFISA HABARI, MAMLAKA YA HALI YA HEWA TANZANIA
Share This
Previous Post
Next Post

Pellentesque vitae lectus in mauris sollicitudin ornare sit amet eget ligula. Donec pharetra, arcu eu consectetur semper, est nulla sodales risus, vel efficitur orci justo quis tellus. Phasellus sit amet est pharetra

0 comments: