Monday, August 28, 2017

Msaada wa haraka kusaidia wakimbizi wahitajika

ad300
Advertisement
Shirika la Umoja wa Mataifa la Mpango wa Chakula Duniani (WFP), limelazimika kupunguza mgao wa chakula kinachotolewa kwa wakimbizi 320,000 wanaoishi katika kambi za Mtendeli, Nduta na Nyarugusu mkoani Kigoma kaskazini magharibi mwa Tanzania kwa sababu ya upungufu wa fedha.
Imeelezwa kuwa chanzo ni uhitaji wa haraka wa jumla ya Dola za Marekani milioni 23.6, kuanzia sasa hadi Desemba mwaka huu, ili WFP imudu kuendelea kutoa mgao unaokidhi mahitaji ya chakula na lishe kwa wakimbizi wanaoishi nchini Tanzania.
Akizungumza mkoani Kigoma jana, Michael Dunford ambaye ni Mwakilishi wa WFP hapa nchini, alisema shirika lao hugawa vyakula vya aina tano tofauti kwa wakimbizi ambao kimsingi wanatoka Burundi na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo.
Alisema vyakula hivyo ni pamoja na unga wa mahindi, kunde, Nafaka Kuu, mafuta ya mbogamboga na chumvi na kwamba kwa sababu ya upungufu wa fedha, aina zote tano za vyakula kwa Agosti zimekidhi asilimia 62 ya kiasi cha kalori 2,100 zinazopendekezwa kitaalamu kutosha mahitaji ya mtu ya siku.
“Pasipo mwitikio wa haraka kutoka wa wahisani, itakuwa lazima kupunguza mgao kwani akiba ya chakula inapungua kwa kasi sana,” alisema Mwakilishi wa Nchi wa WFP Tanzania Michael Dunford.
Pia aliongeza: “Wakati ambapo WFP inashukuru sana kwa msaada uliokwishatolewa hadi sasa, tunatoa wito ili wahisani waitikie haraka na kuwasaidia wakimbizi na kutoa fedha zaidi ili tugawe mgao kamili na kuzuia athari mbaya zisidumu kwa muda mrefu.”
Alisema kupunguza mgao kunasababisha matatizo mengi yanayoweza kubadili vibaya maisha ya wakimbizi. Kupunguza kiasi cha kalori na msaada wa lishe kunaweza kusababisha utapiamlo mkali na kuongeza uwezekano wa kupata magonjwa. 
Licha ya aina hizo tano za vyakula, Shirika la WFP pia hugawa vyakula vya moto kwa wakimbizi mara baada ya kuwasili, mgao wa chakula cha nyongeza kwa wanawake wajawazito na wanawake wanaonyonyesha na msaada wa chakula kwa wagonjwa waliolazwa hospitalini na kwa watu wanaoishi na VVU/UKIMWI.
Hadi sasa vyakula vya moto vinavyogawiwa kwa wakimbizi wanaoingia nchini na programu ya chakula cha nyongeza havijaathiriwa na punguzo la sasa la mgao.
Share This
Previous Post
Next Post

Pellentesque vitae lectus in mauris sollicitudin ornare sit amet eget ligula. Donec pharetra, arcu eu consectetur semper, est nulla sodales risus, vel efficitur orci justo quis tellus. Phasellus sit amet est pharetra

0 comments: