Sunday, August 20, 2017

IPTL, PAP zaigeuzia kibao Standard Chartered

ad300
Advertisement
Kampuni za  Independent Power Tanzania (IPTL) na Pan African Power Solutions (T) Limited (PAP), zimewasilisha maombi  mahakamani kutaka kampuni za Standard Chartered Bank Hong Kong Limited na Standard Chartered Bank Malaysia Berhard ziamriwe kuweka dhamana ya sh. bilioni 50.



IPTL na PAP zimewasilisha maombi hayo wiki iliyopita, katika Mahakama Kuu, Kitengo cha Biashara ambayo yanaungwa mkono na hati ya kiapo cha Wakili wao, Joseph Makandege.



Katika maombi hayo namba 241 ya mwaka huu, IPTL na PAP wanaiomba mahakama hiyo, kuziamuru benki hizo kuweka dhamana ya sh. bilioni 50 kabla ya kusikiliza shauri lililofungiliwa kupinga kusajiri hukumu ya Uingereza ambayo inazitaka kampuni hizo kulipa benki hizo malipo ya Dola za Marekani 168,800,063 (zaidi ya sh. bilioni 376).



Maombi hayo yamepangwa kusikilizwa Oktoba 10, mwaka huu, mbele ya Jaji Barke Sahel, ambaye anasikiliza shauri la kupinga kusajiriwa kwa hukumu hiyo iliyotolewa na Mahakama Kuu ya Biashara ya Uingereza.



Kupitia hati yake ya kiapo, Makandege anadai benki hizo mbili ni mali za kigeni na zimesajiliwa nchini China na Malaysia. Pia anadai benki hiyo hazina mali yoyote Tanzania inayoweza kufidia gharama zitakazotumiwa na kampuni hizo kuendesha shauri hilo hapa nchini.



Aidha, anadai wakili anayeziwakilisha benki hizo ameshindwa kuonyesha mahakamani au kwa wateja wake uhalali wa kuendelea kusimamia shauri hilo au kufungua mashauri yoyote kwa niaba ya benki hizo.



Makandege anadai hakuna maofisa wa juu wa benki hizo waliotia saini nyaraka au kumbukumbu zilizowasilishwa mahakama kupinga shauri hilo, hivyo itakuwa vigumu kwa IPTL na PAP kuwataka maofisa hao kuwajibika kwa kile kitakachotokea baadae.



“Hata nchi kule ambazo benki hizo zilikotoka hazina mikataba au utaratibu na Tanzania wa kutekeleza hukumu zinazotolewa na mahakama za nchi hizo hapa nchini, kitendo ambacho  kinaweza kuzihakikishia IPTL na PAP kulipwa gharama watakazozitumia baada ya shauri hilo kufika mwisho.



Katika hati yake ya kiapo, Makandege anafafanua kiwango cha fedha kinachodaiwa na benki hizo dhidi ya  wateja wake (IPTL na PAP) ambacho ni Dola za Kimarekani 168, 800,063 (sawa na sh. 376,424,142,274), ni kikubwa ambapo inahitajika gharama kubwa na haijaonyeshwa kama wateja wake wamesamehewa kulipa gharama ya kujitetea.



Anadai benki hizo zimekuwa na mwenendo wa kubadili misimamo na wakati mwingine kuondoa au kufuta mashauri waliyoyafungua mahakamani, jambo ambalo limekuwa likiwasababishia walalamikiwa  kuingia gharama kubwa za kujitetea bila msingi wowote.



Wakili huyo anadai  hukumu ya nje inayotaka kusajiriwa imeghubikwa na makosa mengi, jambo ambalo linasababisha kuwepo na uwezekano mkubwa wa kutokubaliwa na mahakama za hapa nchini.



Makandege anadai wakati  IPTL, PAP na VIP Engineering and Marketing Limited zilipokuwa zinapambana Uingereza ziliamriwa kuweka dhamana kwa ajili ya gharama za benki hizo kujitetea kwa kuwa kampuni hizo hazisajiriwa huko na wala hazina  mali yoyote inayoweza kufidia gharama hizo.



Katika shauri la msingi, IPTL na PAP wanaiomba mahakama hiyo kutengua amri iliyotolewa Februari 9, mwaka huu, kusajiri hukumu iliyotolewa na  Mahakama Kuu ya Malkia Uingereza, Idara ya Mahakama ya Biashara ya Novemba 16, mwaka jana kuhusu malipo hayo.



IPTL na PAP wanaiomba mahakama itamke hukumu ya kigeni iliyosajiliwa mbele ya Jaji Sahel haisajiliki na wala haitekelezeki nchini Tanzania.


Share This
Previous Post
Next Post

Pellentesque vitae lectus in mauris sollicitudin ornare sit amet eget ligula. Donec pharetra, arcu eu consectetur semper, est nulla sodales risus, vel efficitur orci justo quis tellus. Phasellus sit amet est pharetra

0 comments: